Thursday, May 9, 2013

MGOSI AJINADI SIMBA,YANGA

Mshambualiaji nyota wa zamani wa timu za Simba na Taifa Stars, Mussa Hassani Mgosi anayeichezea kwa sasa JKT Ruvu, amesema yupo tayari kutua katika timu yoyote ikiwamo Simba na Yanga, mradi aridhishwe na masilahi atakayoafikiana na klabu husika.

Aidha, mshambuliaji huyo alisema amefurahi mno kuisaidia JKT Ruvu kunusurika kushuka daraja, lakini amekiri kwamba klabu hiyo haikuwa na msimu mzuri mwaka huu kwa namna ilivyoyumba na kupoteza makali iliyokuwa nayo kwa misimu kadhaa ya nyuma.

Mgosi aliyewahi kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Motema Pembe ya DR Congo, alisema kwa vile mkataba wake wa mwaka mmoja na JKT Ruvu unamalizika mwisho wa msimu huu, atakuwa huru kutua katika klabu yoyote itakayomhitaji.

Mgosi alisema hatajali ni timu gani itakayomhitaji kwa msimu ujao, mradi wakubaliane kimasilahi kwa kuwa yeye ni mwanasoka na ajira yake inategemea mchezo huo.

Aliongeza kuwa hata kama JKT Ruvu itamhitaji aendelee kubaki hatakuwa na pingamizi kwa vile ni moja ya timu anazozipenda na alishawahi kuichezea zamani kabla ya kurejea safari hii na kuitumikia tena.

"Niko tayari kutua kokote kwa msimu ujao, sitabagua timu hata kama ni Mbeya City, Ashanti, Simba au Yanga, muhimu ni masilahi tu," alisema.

Mfungaji bora huyo wa zamani wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara na michuano maalum iliyofanyika China mwaka jana, alikiri ligi ya msimu huu ilikuwa ngumu na isiyotabirika japo anasikitika vibali kumkwamisha kuishiriki tangu mzunguko wa kwanza baada ya kurejea kutoka Congo.



Source:Nipashe



0 comments:

Post a Comment